DC Hapi aagiza mratibu wa TASAF Kinondoni kuvuliawa cheo

Alli Hapi
Kaya 1,397 zisizo na sifa wilayani Kinondoni zimepokea fedha za mradi wa kuwezesha kaya masikini (TASAF).

Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Ally Hapi amesema kwa mujibu wa uhakiki uliofanywa na TASAF hivi karibuni, imebainika kuwa kaya 517 ziliorodheshwa katika orodha ya wanaostahili kupewa fedha za msaada, na kupewa zaidi ya milioni 180 katika awamu tofauti, hali zao kiuchumi zinaridhisha na kwamba zimeondolewa katika mradi huo.

Pia, Hapi amesema uhakiki huo umebaini kuwa kaya 537 zilizopokea fedha za msaada zaidi ya sh. 266 Milioni hazijulikani makazi yake katika wilaya hiyo, wakati kaya 59 zikibainika hazina makazi huku 15 zikichukua fedha hizo zaidi ya mara moja na 265 zilihama makazi.

Kufuatia ubadhirifu huo wa fedha, Hapi amemuagiza mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni kumvua cheo Mratibu wa TASAF wilayani Kinondoni Onesmo Kweyamba kwa kushindwa tekeleza majukumu yake na kuruhusu baadhi ya watumishi wa serikali, wafanyabiashara na kaya zenye uwezo kupata fedha za msaada.

Aidha, ameagiza vyombo vya dola kwa kushirikiana na TASAF kufanya uhakiki tena na kwamba kata itakayobainika kuwa imeorodhesha kaya zenye uwezo kwa ajili ya kupewa fedha hizo, mwenyekiti wake anachukuliwa hatua za kisheria.

Amesema majina ya kaya zisizo na sifa yatabandikwa katika maeneo husika ili zijijue kisha kurudisha fedha zote ilizopokea.

No comments