Meneja
Uhusiano wa Mfuko wa Pensheni wa PPF, Lulu Mengele, (kulia), akiwasaidia
wanakijiji hawa wa Ikwiriri, Wilayani Rufiji mkoani Pwani, kutuma michango kwa
njia ya mtandao wa simu, wakati wa kuandikisha wanachama chini ya mpango wa
Wote Scheme kwenye chuo cha Maendeleo ya Jamii, Ikwiriri, Oktoba 3, 2016. Takriban wanakijiji 395
wakiwemo, wakulima, wafuga nyuki, wavuvi na waendesha bodaboda, wamekabidhiwa
kadi za uanachama kupitia mpango huo unaoruhusu mtu yeyote aliye kwenye sekta
rasmi na isiyo rasmi kujiunga kwa kuchangia kila mwezi kima cha chini shilingi
20,000.
Na Mwandishi Wetu, Ikwiriri
MFUKO
wa Pensheni wa PPF, kupitia mpango wa Uchangiaji wa Hiari, “Wote Scheme”,
umesajili karibu wanachama 400 huko
Ikwiriri wilayani Rufiji mkoa wa Pwani.
Akizungumza
na waandishi wa habari wakati wa zoezi la usajili na ugawaji kadi za uanachama
kwenye viwanja vya chuo cha Ufundi Ikwiriri, (IFDC), Oktoba 3, 2016, Meneja wa
PPF Kanda ya Temeke, Erica Meshack Sendegeya, alisema, wanakijiji hao wajasiriamali walihamasika
kujiunga na mpango huo baada ya Kanda yake kutoa elimu juu ya umuhimu wa
wananchi kujiunga na Mfuko huo kwani kuna manufaa mengi.
“Tuliwaeleza,
mpango huu wa Wote Scheme umebuniwa ili kutoa fursa ya wananchi walioajiriwa au
waliojiajiri wenyewe, wakiwemo wakulima, wavuvi, wafugaji, Boda boda na mama lishe, kujiunga na Mfuko kwa kuchangia
kima cha chini cha shilingi 20, 000 kila mwezi. “Fedha hizo unaweza kuzitoa kwa
mkupuo au kwa awamu kulingana na uwezo wa mwanachama,” alifafanua Sendegeya.
Akielezea
faida za kuwa mwanachama, Meneja huyo alisema, “Mwanachama atafaidika na fao la
Afya ambapo atapatiwa bima ya afya kupitia NHIF baada ya kuchangia shilingi
elfu 60,000 tu.” Alisema na kuongeza kuwa faida nyingine ni pamoja na
mwanachama kujipatia mkopo wa maendeleo ambapo sharti kuu la kupata mkopo huu
ni mwanachama kuchangia Mfuko kwa kipindi cha miezi sita, mkopo wa elimu,
lakini pia fao la uzeeni, alisema Meneja huyo.
Kuhusu
namna mwanachama anavyoweza kuchangia baada ya kujiunga na Mpango huo, Meneja
Uhusiano wa PPF, Lulu Mengele alisema, “Kuna njia rahisi ya kuwasilisha
michango, ambayo ni kutumia mitandao ya simu, Airtel Money, Tigo Pesa na
M-Pesa.” Alisema.
Baadhi
ya wanakijiji waliojiunga na Mpango huo, wameipongeza PPF kwa kutoa elimu
ambayo imewafanya wajiunge na Mfuko huo na ni matarajio yao utasaidia kuboresha
shughuli zao.
“Mimi
ni mfuga nyuki, kilichonivutia ni jinsi Mfuko huu unavyoweza kutoa mikopo ya
maendeleo,” alisema Erasto Joseph, ambaye pia ni mwalimu wa shule.
Naye
Ishara Ibrahim ambaye ni mkulima, alisema, ni matarajio yake kuwa kujiunga na
PPF, basi ataweza kumudu kupata huduma ya afya kupitia Bima ya Afya.” Alisema.
No comments