Mkuu wa wilaya ya Kibaha aweka kipindi cha mpito kwa wafugaji

 http://www.simamia.com/wp-content/uploads/2015/09/mshama.jpg

MKUU wa wilaya ya Kibaha mkoani Pwani Asumpter Mshama ameweka kipindi cha mpito kwa wafugaji wa wilaya hiyo kutoingiza mifugo kwenye mashamba ya wakulima wakati serikali ikiangalia namna ya kumaliza migogoro baina yao na wakulima.

Amesema hayo ofisini kwake mjini Kibaha wakati alipokutana na viongozi wa wafugaji baada ya agizo lake la kuwataka wafugaji kupunguza mifugo yao pia kwenda kwenye maeneo ambayo yalitengwa kwa ajili yao ambapo alitoa mwezi mmoja toka Septemba 15 hadi Oktoba 15 mwaka huu kwa wafugaji kwenda kwenye maeneo yao  kupunguza migogoro baina yao na wakulima.

Alisema kuwa katika kipindi hicho cha mpito kabla ya maamuzi mengine hayajachukuliwa hawapaswi kulisha mifugo kwenye mashamba ya wakulima na endapo watafanya hivyo ngombe watakaoingia kwenye mashamba watagawana na wakulima walioharibiwa mazao yao.

Naye Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini Hamoud Jumaa alitaka maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya wafugaji yaainishwe ili kupunguza migogoro hiyo ambayo kwa sasa imekithiri wilayani humo.

Jumaa alisema kuwa endapo maeneo hayo yataainishwa itasaidia kupunguza mifugo kuingia kwenye mashamba ya wakulima na kusababisha uvunjifu wa amani.

Kwa upande wake mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Kibaha Tatu Seleman aliwataka wafugaji kukaa kwenye maeneo yao ambayo walitengewa.

Seleman amesema kuwa maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya wafugaji wenyewe hawayatumii na kutaka kukaa na wakulima jambo ambalo limeleta sintofahamu kwa pande hizo mbili.

Naye katibu wa chama cha Wafugaji nchini Magembe Makoye alisema kuwa imefika wakati wafugaji kukubali mabadiliko kwa kufuga kisasa kwa kutegemea ukubwa wa eneo.

Makoye amesema kuwa kwa sasa mifugo imekuwa ni mingi huku eneo la kufugia likiwa dogo hali ambayo inasababisha migogoro ya mara kwa mara baina ya wakulima na wafugaji pia aliomba kuwe na ushirikishwaji wa maamuzi ya namna ya ufugaji.

Naye mfugaji Amerika Chamiti amesema kuwa ni vema mipaka iliyowekwa baina ya wakulima na wafugaji ionyeshwe ili kupunguza migogoro hiyo kwani pande hizo zimekuwa zikiingiliana.

Chamaiti amesema kuwa mipaka ndiyo itakayosaidia kuanisha eneo la kila upande kwani Halmashauri ilitenga maeneo hayo karibu kila kijiji lengo likiwa ni kila mtu akae kwake na asiingie kwa mwenzake.

Kikao hicho kimekuja baada ya mkuu wa wilaya hiyo Asumpter Mshama kutoa mwezi mmoja hadi ifikapo Oktoba 15 wafugaji wote wawe wamekwenda kwenye maeneo waliyopangiwa pamoja na kupunguza mifugo ili kuepusha migogoro baina ya wakaulima na wafugaji.  

No comments