Thursday, April 28, 2016 Serikali Kuwasilisha Mswada wa wa sheria wa Ndoa.

Serikali imejiandaa kuleta Muswada wa Sheria bungeni kutoa haki ya kusoma
kwa watoto wote wa kike na kiume wa shule za msingi, sekondari na
kutoruhusiwa kuoa au kuolewa.

Aidha, Waziri wa Katiba na Sheria, Dk Harrison Mwakyembe amesema serikali
inaendelea kukamilisha utaratibu wa kupata maoni ya wananchi kuhusu
marekebisho ya Sheria ya Ndoa na kutungwa kwa Sheria mpya ya Mirathi na
Urithi kuondokana na mkanganyiko uliopo kuhusu sheria hiyo.

Bunge lilielezwa hayo jana mjini Dodoma wakati waziri huyo akijibu swali la
nyongeza la Mbunge wa Ileje, Janeth Mbene (CCM) aliyehoji ni lini serikali
itaanza maandalizi ya kuchukua maoni juu ya kufanya marekebisho sheria ya
ndoa ya mwaka 1971.

Akijibu swali hilo, Dk Mwakyembe alisema hatua za awali zimeshaanza
kuchukuliwa na wizara hiyo ili kupata maoni ya wananchi juu ya marekebisho
ya sheria hiyo ya ndoa ya mwaka 1971 na kutungwa kwa sheria mpya ya
mirathi na urithi.

Alisema serikali ina nia ya dhati ya kufanyia marekebisho sheria ya ndoa na
kwamba mchakato huo ulisitishwa kwa kuwa Tume ya mabadiliko ya Katiba
ilikuwa ikikusanya maoni kuhusu mabadiliko ya katiba , hivyo walidhani
wananchi wangetoa pia maoni juu ya sheria hiyo.


Waziri wa Katiba na Sheria  Dkt.Harrison Mwakyembe.

No comments