Wazazi watakaobainika kuwaficha watoto ndani bila kuwaandikisha madarasa ya awali na msingi kuchukuliwa hatua
Na.Vero Ignatus, Arusha
SERIKALI imesema kuwa itawachukulia hatua kali na za kisheria wazazi au walezi watakaobainika kuwaficha ndani watoto wao bila kuwaandikisha madarasa ya awali na msingi kwani kuwaficha watoto hao kunawanyima haki za kupata elimu bure. Aidha hata kwa wale watoto wenye ulemavu nao wanapaswa kupelekwa kwenye shule maalum zinazohusika na kutoa huduma za walemavu ili waweze kunufaika na elimu kama ilivyo kwa watoto wengine katika jamii badala ya kufichwa ndani. Hayo yalisemwa jana na mkuu wa wilaya ya Arusha Gabriel Daqqaro alipokuwa akizungumza na blog hili kuhusiana na umuhimu wa wazazi kutumia fursa ya kuwaandikisha watoto wao kuanzia ngazi ya awali ,msingi na kidato cha kwanza ili kuwawezesha wanufaike na elimu bila malipo. Alisema kuwa kwa sasa wazazi au walezi wanapaswa kutumia fursa iliyopo kwa kuwaandikisha watoto wao mashuleni kuanzia ngazi za awali na kwamba wale wazazi wote ambao watabainika kuwaficha watoto wao majumbani watachukuliwa hatuamza kisheria. "Shule zimeshafunguliwa na kwa sasa uandikishaji unaendelea hadi mwezi machi hivyo wazazi watumie fursa hii ya elimu bila malipo kwa kuwaandikisha watoto wao na kwa wale ambao wamekuwa na tabia ya kuwaficha watoto wao ndani waache mara moja kwani tutawachukulia hatua za kinidhamu "-alisema Daqqaro. Alidai kuwa hata kama wazazi wana watoto wenye ulemavu hawapaswi kuwaficha ndani bali wawatoe na kuwaandikisha kwenye shule maalum kama ilivyo shule ya Meru kwa wale wenye ulemavu mbali mbali kwani endapo watagundulika watatumia vyombo vya dola kuwachukulia hatua kali wazazi hao. Aliongeza kuwa serikali ya awamu ya tano imeshatimiza ahadi ya elimu bure na kwamba kwa ngazi ya wilaya wameshamaliza ujenzi wa madarasa ambayo yalikuwa yameonekana ni changamoto ya kukwamisha swala la elimu katika baadhi shule na kwamba kazi kubwa imebakia kwa wazai kuhakikisha watoto wao wanaandikishwa na kuhudhuria mashuleni. |
No comments