Wasanii wa filamu wa china kutangaza vivutio vya utalii vya Tanzania
WATANZANIA wametakiwa kuendeleza ukaribu kwa wageni na kuhifadhi
vivutio vya utalii ili kushawishi wageni wengi kuja nchini kwa utalii ambao una
nafasi kubwa ya kuitangaza Tanzania ulimwenguni.
Akizungumza kwa niaba ya Waziri Maliasili na Utalii, Profesa
Jumanne Maghembe, Mwenyekiti wa Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) Jaji Mstaafu
Thomas Mihayo, katika hafla ya kuwaaga wasanii maarufu wa filamu kutoka China
waliokuja nchini kwa shughuli za kisanii na kuangalia vivutio vya utalii kuwa
Tanzania ni tajiri kwa vivutio vyingi vya utalii.
“Bado nchi yetu inajipambanua kwa amani duniani, wageni wengi
wanavutiwa kuja kufanya shughuli mbalimbali za kisanii na kujifunza utamaduni
wetu kutokana na sifa kubwa ya amani na utulivu, tuzilinde tunu hizi ili waje
wengi zaidi,” alisema.
Jaji Mihiayo alisema kwa
upande wa utalii Tanzania imenufaika kupata wageni hao ambao miongoni mwao ni
wasanii maarufu katika nchi yenye watu zaidi ya bilioni 1.2.
“Siyo Wachina wote wanaijua Tanzania lakini kupitia
mabalozi hawa tutaendelea kupokea wageni wengi kutoka huko,” aliongeza Jaji
Mihayo, na kuwaomba wasanii hao kuwa mabalozi wazuri watakaporudi nchini kwao.
Katika hafla hiyo iliyofanyika usiku wa kuamkia jana kwenye ukumbi
wa Makumbusho ya Taifa jijini hapa, kulikuwepo na wasanii maarufu saba
walioambatana na wasaidizi wao ambao kwa pamoja walikuwa 150.
Jaji Mihayo alisema wasanii hao walikuwepo Tanzania kwa siku 15
kwa shughuli ya uigizaji kwa ajili ya mfululizo wa filamu kupitia Hunan
Television. Maeneo waliyotembelea ni Ngorongoro, Serengeti, Visiwa vya Pemba na
Dar es Salaam.
Msanii maarufu nchini China, Li-Yu anayeigiza nafasi ya mpambanaji
dhidi ya rushwa katika tamthilia ya ‘In the name of the people’ inayoendelea
sasa nchini humo kupitia Hunan Television, alisema wiki mbili walizokaa
Tanzania hawatazisahau kutokana na aina ya watu waliokutana nao wenye upendo na
huruma.
“Tumekutana na mazingira murua, watu murua katika nchi nzuri yenye
kuvutia, tumefurahia kila hatua tuliyopiga na sekunde iliyopita. Kitu ambacho
sitakisahau nikiondoka katika ardhi hii ni umuhimu wa kutunza wanyamapori,
Tanzania ina wanyama wazuri wa kuvutia sijawahi kuona maishani mwangu.
“Nitabeba jukumu la kuhifadhi mazingira na wanyamapori, kwa sababu
nimebaini ni kitu kinachoburudisha macho. Tumefika visiwa vya Pemba hakika kuna
fukwe nzuri za kupumzisha akili baada ya kazi nzito, hakika tumechagua eneo
zuri la kuchukua vipande vya filamu tutakayowaonyesha Wachina wenzetu,” alisema
Bwana Li-Yu.
“Tanzania ni mahali
panapovutia macho kama uchawi na China ni nchi yenye watu wengi wenye utamaduni
mbalimbali ambao asilimia kubwa wanapenda kutembelea maeneo mbalimbali duniani,”
Alisema Jaji Mihayo.
Alisema muunganiko huu utasaidia kuongeza idadi ya watalii nchini
kama Mamlaka ya Utalii China (CNTA) ilivyoorodhesha mataifa saba muhimu kwa
utalii duniani na Tanzania ikawemo basi tutahakikisha hatuwaangushi.
”
Wakati hafla hiyo, TTB kupitia Mwenyekiti wake wa Bodi walitoa zawadi za shuka za Kimaasai kwa wasanii hao
kama kumbukumbu kwao.
“Kwa utamaduni wa Kiswahili
unapotembelewa na mgeni unamweleza kuwa ikiwa kuna lolote tulilowakosea
naombeni mliache hapahapa na tutalishughulikia ipasavyo ili mkija siku nyingine
mtakuta limerekebishwa. Nanyi tunaomba mfanye hivyo, mabaya yaacheni hapahapa
ondokeni na mazuri tu.” Alisema.
Katika watu maarufu saba waliotajwa katika ujumbe huo kuna wasanii
wa filamu, mshindi wa mashindano ya Olympic na mshindi wa mashindano ya urembo
China.
Vipande vya filamu walivyoigiza katika maeneo mbalimbali ya
kitalii nchini vitatumika katika mfululizo wa tamthilia inayoonyeshwa Hunan TV,
ambayo ina watazamaji zaidi ya milioni 800 katika nchi hiyo yenye watu
wanaofikia bilioni 1.2.
No comments