Polisi Arusha waeleza chanzo cha vifo katika ajali ya basi la Shule ya Lucky Vicent

Ajali ya basi la Shule ya Lucky Vicent iliyotokea Mei 6, 2017 katika eneo Rhotia Marera, Wilaya ya Karatu Mkoani Arusha na kusababisha vifo vya wanafunzi 32, walimu wawili na dereva mmoja vifo hivyo vingeweza kupungua kama kama basi hilo lingekuwa na mikanda na kila mmoja akaufunga kabla ya kuanza safari.

Kamanda wa Polisi Msaidizi wa Mkoa wa Arusha, Yusuf K Ilembo amesema kuwa wengi waliofariki katika ajali ile ni kutokana na kuumia ndani ya mwili kulikosababishwa na kugongana wakati ajali ilipotokea.

Wangekuwa wamefunga mikanda, huenda vifo vingekuwa vichache au visiwepo kabisa alisema. Aidha Kamanda Ilembo alisema pia, hata mwendo kasi wa basi hilo ulichangia kupata ajali na kupelekea vifo vya watu 35.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha Charles Mkumbo alieleza kuwa gari aina ya Mitsubish Rosa lililohusika katika ajali iliyoua watu 35, lilikuwa limebeba abiria 38 wakati uwezo wake ukiwa ni abiria 30 tu.

Katika ajali hiyo waliosalimika ni abiria watatu tu kati ya 38 waliokuwamo ndani ya basi hilo wakati linapata ajali.

Kwa sasa tutatilia mkazo ukaguzi wa magari yote yanayotumika kusafirisha wanafunzi ili kujua kama yana uwezo na sifa za kutumika kwa shughuli hiyo. Pia maafisa wetu watazitembelea shule mbalimbali zenye magari ya kusafirisha wanafunzi ili kutoa elimu kuhusiana na usalama wa barabarani,” alisema.

Ilembo aliongeza kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya uongozi wa shule zitakazobainika kuwa na mabasi yasiyo na ubora na kiwango cha kuwasafirisha wanafunzi.

Alithibitisha kuwa Mmiliki wa Shule ya Lucky Vicent, Innocent Moshi anashikiliwa na jeshi la Polisi Arusha kwa ajili ya mahojiano.

“Bado yupo mikononi mwa polisi kwa ajili ya mahojiano kuhusiana na ajali iliyotokea. Tunataka kujua kama basi lile lilikuwa na viwango vya kuwasafirisha wanafunzi,” alisema.

Wakuu wa Shule mbalimbali jijini Arusha wamethibitisha kuwa polisi na maafisa wa usalama barabarani wamefika katika shule zao ili kuyafanyia ukaguzi magari yote yanayotumika kusafirisha wanafunzi katika shule hizo.

Mkuu wa Shule ya Lady of Mercy iliyoko Kimandolu, Irene Mogusu alieleza kuwa siku ya Jumatano maafisa wa usalama barabarani walifika katika shule yake kwa ajili ya ukaguzi.

Inakadiriwa kuwepo kwa shule binafsi za awali, msingi pamoja na sekondari zaidi ya tisini katika mkoa wa Arusha peke yake. Na magari mengu ya shule hizo yana rangi ya njano.

No comments