Fistula: Janga nyamavu ambalo licha ya kutibika linadhuru wanawake 500,000 duniani

United NationsFistula: Janga nyamavu ambalo licha ya kutibika linadhuru wanawake 500,000 duniani
Fistula ya uzazi ni ugonjwa unaotibika kabisa ambao huathiri zaidi ya wanawake 500,000 duniani kote.
© UNFPA/Ollivier Girard
 
Fistula ya uzazi ni ugonjwa unaotibika kabisa ambao huathiri zaidi ya wanawake 500,000 duniani kote.

Siku 5 – ni muda ambao Dah msichana mwenye umri wa miaka 14 kutoka Côte d’Ivoire alitumia kujifungua ili awe mama. Mtoto alizaliwa akiwa amefariki na Dah alipata fistula ya uzazi.

Miaka 16 – Huo ndio muda Dah aliishi na jeraha la Fistula alilopata baada ya uchungu wa muda mrefu kwenye kujifungua. Alifanyiwa upasuaji mara nane kabla ya kufanikisha matibabu ya fistula.

Miili ya wanawake inakuwa uwanja wa vita – si tu kupitia ukatili wa kingono bali pia kwa kunyimwa kwa makusudi haki na huduma za afya ya uzazi _ Sima Bahous

Katika kutambua wanawake zaidi ya 500,000 kama Dah ambao wanalazimika kuvumilia hali hii inayoweza kutibika kwa urahisi, Siku ya Kimataifa ya Kukomesha Fistula ya Uzazi imeadhimishwa leo Ijumaa ya tarehe 23 Mei 2025.

Fistula ya uzazi ni hali ya kiafya ambalo ni tundu dogo kati ya njia ya uzazi na kibofu cha mkojo , linalosababisha kuvuja kwa mkojo au kinyesi.

Kaulimbiu ya mwaka huu, “Afya yake, Haki yake: Kuweka msingi wa Mustakabali bila Fistula”, inalenga kusukuma mbele juhudi za kutokomeza fistula ifikapo mwaka 2030.

“Miili ya wanawake inakuwa uwanja wa vita – si tu kupitia ukatili wa kingono bali pia kwa kunyimwa kwa makusudi haki na huduma za afya ya uzazi,” amesema Sima Bahous, Mkurugenzi Mtendaji wa UN Women, shirika la Umoja wa Mataifa la Kushughulikia Masuala ya Wanawake.

‘Janga la kimya kimya’

Fistula mara nyingi husababishwa na uchungu wa uzazi unaochukua muda mrefu au kuwa mgumu. Zaidi ya wanawake nusu milioni walio na hali hiyo wanaishi katika nchi maskini.

Wanawake wengi waliopata fistula hupitia hali ya kujitenga na jamii kutokana na kuvuja kwa mkojo au kinyesi – jambo linaloweza kusababisha msongo wa mawazo na umaskini mkubwa.

Kambiré, mfanyabiashara mdogo kutoka Bouna, nchini Côte d’Ivoire, aliishi na fistula ya uzazi kwa miaka 23. Alifanikiwa kupata mtoto mwingine kabla ya kupata msaada wa matibabu.

“Nilijitenga kwa sababu ya fistula,” amesema. “Nisingeweza kukaa kwa muda mrefu kwa hofu ya kulowana.”

Alifahamu kuwa hali hiyo inatibika kupitia kipindi cha redio, na ndipo alipohamasika kwenda katika hospitali inayosaidiwa na shirika la afya ya uzazi la UN (UNFPA) kupata matibabu. Sasa anamiliki biashara ndogo ya utengenezaji vyungu.

Kambiré alikuwa na fistula ya uzazi kwa miaka 23 na sasa anamiliki biashara yake ya kutengeneza sufuria.
© UNFPA/Ollivier Girard
 
Kambiré alikuwa na fistula ya uzazi kwa miaka 23 na sasa anamiliki biashara yake ya kutengeneza sufuria.

Hali inayozuilika na kutibika kabisa

UNFPA imeweka lengo la kutokomeza fistula ifikapo mwaka 2030 – jambo linalowezekana kwani, kiafya, ni hali inayoweza kuzuilika na kutibika kabisa.

Kati ya mwaka 2003 na 2024, UNFPA ilisaidia zaidi ya upasuaji wa fistula 150,000, ambapo 4,400 kati ya hizo zilifanyika Côte d’Ivoire kwa wanawake kama Dah na Kambiré.

Catherine, mama wa watoto wawili kutoka Bouna, pia alipata msaada wa matibabu kutoka hospitali inayoungwa mkono na UNFPA.

“Sasa kwa kuwa nina afya, nina furaha. Naweza kuendesha biashara yangu na kutumia muda na marafiki,” amesema.

Nafasi ya wakunga na wanawake wenyewe katika kutokomeza Fistula

Hata hivyo, fistula ya uzazi imeendelea kuwepo duniani kote kutokana na tofauti katika mifumo ya afya ya dunia.

UNFPA inasema wakunga ni muhimu sana katika kuzuia fistula na madhara mengine ya uzazi. Hata hivyo, kuna uhaba wa wakunga zaidi ya 900,000 duniani, ambapo 500,000 kati yao wanahitajika Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara.

Elimu ya afya ya uzazi na uwezeshaji wa wanawake ni muhimu vilevile katika kushughulikia na kuzuia fistula ya uzazi.

“Ngome bora kabisa tunayoweza kuwapatia wanawake na wasichana ni nguvu yao wenyewe, sauti zao na uongozi wao,” amesema Bi. Bahous.

Mitandao ya mshikamano

Baada ya Dah kupata matibabu ya fistula, alianza biashara ya vyakula vya msimu kama Kambiré, ambapo huandaa na kuuza mazao.

Pia alijiunga na wanawake wengine waliopona fistula kutoka Bouna kuhamasisha jamii na kupunguza unyanyapaa.

“Wanawake wanapokuwa viongozi, hawalindi tu nafsi zao bali pia familia na jamii zao … Matokeo yake ni ya kubadilisha maisha,” amesema Bi. Bahous.

No comments