Benki ya CRDB yawakaribisha Wanahisa kwenye Mkutano Mkuu wa 30
Benki ya CRDB yawakaribisha Wanahisa kwenye Mkutano Mkuu wa 30
Arusha
14 Mei 2025 - Benki ya CRDB imewataka wanahisa wake kujitokeza kwa
wingi kushiriki katika Mkutano Mkuu wa 30 wa Wanahisa, unaotarajiwa
kufanyika Jumamosi, tarehe 17 Mei 2025, katika Kituo cha Kimataifa cha
Mikutano cha Arusha (AICC), ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 30
ya mafanikio tangu kuanzishwa kwa benki hiyo.
Taarifa
hiyo imetolewa leo katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika
kwenye hoteli ya Gran Meliá, jijini Arusha, ambapo Benki ya CRDB pia
ilizindua Ripoti yake ya Mwaka 2024, inayoonyesha maendeleo makubwa ya
kifedha, kiutendaji na kijamii yaliyopatikana katika kipindi hicho.
Akizungumza
katika mkutano huo, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB,
Dkt. Ally Laay, amesema kuwa Mkutano Mkuu wa mwaka huu utakuwa wa
kipekee kwani utatanguliwa na semina maalum kwa wanahisa na umma,
itakayofanyika Ijumaa, tarehe 16 Mei 2025, katika ukumbi wa Simba, AICC.
“Semina hii ya kihistoria itakuwa chini ya kaulimbiu yetu ya mwaka huu:
‘Miaka 30 ya Ukuaji wa Pamoja,’ na itafunguliwa rasmi na Makamu wa Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor
Mpango. Ni fursa muhimu ya kutafakari mafanikio yetu ya pamoja,
changamoto tulizozishinda, na mwelekeo wetu wa miaka ijayo,” amesema
Dkt. Laay.
Ajenda
mbalimbali zitajadiliwa katika Mkutano Mkuu wa 30 wa Wanahisa wa Benki
ya CRDB ni pamoja na uchaguzi wa wajumbe wa bodi, kuteua wakaguzi wa
hesabu, kujadili mapendekezo ya maboresho ya Katiba ya Benki, kujadili
na kupokea Taarifa ya Bodi ya Wakurugenzi, na Taarifa ya Hesabu
zilizokaguliwa, pamoja na gawio kwa mwaka 2024 ambapo pendekezo la gawio
la Sh 65 kwa hisa litawasilishwa sawa.
Kwa
upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela
amesema maandalizi ya Mkutano Mkuu wa Wanahisa yamekamilika kwa asilimia
100. Nsekela amesema mkutano huo utafanyika kwa njia mseto “Hybrid
Meeting” ili kutoa fursa kwa wanahisa wengi zaidi kushiriki moja kwa
moja na kwa njia ya kidijitali. “Tumeweka muongozo wa jinsi ya kushiriki
mkutano mkuu kwa njia ya mtandao kupitia tovuti yetu ya www.crdbbank.co.tz,
mitandao yetu ya kijamii, lakini pia maelekezo yametumwa kwa ujumbe
mfupi kwa Wanahisa,” amesema Nsekela huku akiwahakikishia kuwa Benki
hiyo vizuri katika kuhakikisha wanashiriki bila chanagamoto yoyote.
Nsekela
amewahamasisha wanahisa kujitokeza kwa wingi kushiriki katika Mkutano
Mkuu huo wa kihistoria, akisisitiza kuwa uwepo wao ni muhimu kwa ajili
ya kushuhudia mafanikio makubwa yaliyopatikana katika miaka 30.
“Tumejenga taasisi imara inayotoa huduma bora, tumeongeza thamani kwa
wanahisa, na kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya taifa letu. Hii ni
fursa adhimu kwa kila mwanahisa kujivunia sehemu yake katika mafanikio
haya na kushiriki kuamua mustakabali wa benki yetu katika miaka ijayo,”
amesisistiza.






No comments