ZIARA YA MAKAMU WA RAIS WILAYA YA MEATU MKOANI SIMIYU
Makamu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan leo ameendelea na ziara yake katika mkoa wa Simiyu ambapo ameweka jiwe la msingi katika mradi wa ujenzi wa bwawa la maji
kwa ajili ya binadamu na mifugo katika eneo la Mwanjolo, wilayani Meatu mkoani Simiyu.
Bwawa hilo la maji litahudumia wananchi kumi na tatu elfu na mifugo laki moja na elfu nane wa Mwanjolo, mradi huo mpaka kukamilika utatumia shilingi za kitanzania bilioni 1.6 na utahifadhi kiasi cha maji lita 345,129,000.
Makamu wa Rais aliwataka wananchi wa Mwanjolo kulinda vyanzo vya maji na kutunza mazingira.
Akizungumza na Wananchi waliojitokeza kushuhudia uwekaji jiwe hilo la msingi Makamu wa Rais alisema “ Serikali ya awamu ya tano ina dhamira ya dhati ya kuhakikisha huduma ya maji inapatikana
kwa wananchi wote”
Makamu wa Rais aliwapongeza wananchi wa Wilaya ya Meatu kwa kulima pamba kwa wingi ambapo wilaya hiyo inategemea kilo 84 na kuwaahidi wananchi hao kuwa dawa za kuulia wadudu zitapatikana kwa wingi kuanzia mwisho wa mwezi huu kwani serikali imetoa fedha zaidi ya bilioni 9
Makamu wa Rais aliwaambia wananchi hao kuwa barabara zote ambazo ilani ya uchaguzi imeahidi kuzijenga zitajengwa na zile ambazo hazipo kwenye ilani ila zina umuhimu zitaingizwa kwenye
bajeti ijayo.
Wakati huohuo Mbunge wa Jimbo la Kisesa Mhe. Luaga Mpina alisema kuwa kati ya kata 13 ni vijiji vine tu vina maji hivyo alimuomba Waziri wa Maji kusaidia zaidi upatikanaji wa maji.
Waziri wa Maji na Umwagiliaji Mhe. Mhandisi Isack Kamwelwe aliahidi kusimamia kwa ukamilifu upatikanaji wa maji .

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa mradi wa bwawa la maji kwa ajili ya matumizi ya binadamu na mifugo la Mwanjolo wilayani Meatu mkoani Simiyu. (Picha na Ofisi ya Makamu wa Rais)
Waziri wa Maji na Umwagiliaji Mhandishi Isack Kamwelwe akitoa maelezo ya mradi wa ujenzi wa bwawa la maji Mwanjolo kwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan. (Picha na Ofisi ya Makamu wa Rais)











No comments