Vijana tunaopata fursa tutende vema kufungua njia kwa wengine'
Vijana tunaopata fursa tutende vema kufungua njia kwa wengine'

Na .Esther Namuhisa
BBC News, Dar es Salaam
Diana Chando (27) ni mwanasheria na mbobezi wa sera anayependa kugusa maisha ya vijana wenzake. Anasema lengo lake kubwa ni kufanya kazi na kuacha alama kubwa katika maisha yake kwa kubadilisha maisha ya watu.
Diana anasema wakati anasoma chuo kikuu kuna siku alipata fursa ya kuwasilisha mada kwa kuwa mhusika hakuwepo na mgeni rasmi alikuwa balozi kutoka Geneva, Uswisi.
Baada ya uwakilishi mzuri, alipewa fursa ya kwenda kwenye mafunzo ya amani, na ndipo safari yake ya kuwa mhamasishaji wa amani ilipoanza.
Ni binti aliyepata malezi kutoka kwa mama pekee, kwa kuwa baba yake alifariki dunia akiwa mdogo sana.
Diana anajivunia hatua aliyoifikia ya kuwa balozi wa vijana wa Afrika huku akiwa amejiwekea misingi thabiti ya kusimamia malengo yake au ndoto zake kubwa.
“Mama yangu ni mchapa kazi sana, mama amekuwa nguzo kwangu kwa kuwa nimeona kujitoa kwake, uaminifu wake, umahiri wake katika kazi na hata elimu aliyonipatia ni zawadi tosha kwangu.
AUCHANZO CHA PICHA,DIANA
Adabu na uvumilivu ni silaha ya uongozi
Mabinti tuna fursa nyingi sana, ukiwa binti mdogo mwenye malengo makubwa haswa kwenye jarida la uongozi lazima kuwa na kitu kinaitwa ‘adabu’.
Kama huna adabu huwezi kufika popote, kwa sababu kama huna adabu huwezi kujua namna nzuri ya kuongea na watu, hutaacha jina zuri kama huna adabu na hutaacha muonekano mzuri kwa watu kama huna adabu , ni utakuwa tu mwanamke mrembo lakini hamna kitu, adabu ni muhimu sana.”
Diana anasisitiza hilo kwa kuwakumbusha vijana kuwa ule msemo unaosemwa kuwa ‘si kila kikombe cha fursa kinachokuja mbele yako ni cha kwako, ni muhimu kujua kipi cha kwako na kipi sio cha kwako vinginevyo utakula sumu.
Adabu ni msimamo wangu wa kwanza katika kujua fursa yangu iko wapi.
Jambo lingine muhimu ni uvumilivu, sipendi kusikilizwa kwa sababu mimi ni binti. Kuwa mwanamke hakunifanyi mimi nifike sehemu bali naamini kuwa utendaji kazi wangu, akili na kujitoa ndiyo kunanifanya nifike sehemu. Sipendi nipewe kitu kwasababu ni mwanamke, bali napenda kupata kitu kwa kuwa nina weledi wa kukifanyia kazi.
Kuna wanawake wengi wanapewa nafasi katika uongozi lakini hawafanyi chochote, ni wakati sasa kutoangalia kwa sababu wewe ni mwanamke.
Umuhimu wa kujitolea
Mtanzania huyu anayewakilisha vijana wa Afrika Mashariki katika umoja wa Afrika AU amedhamiria kuwa kiongozi atakayeacha alama katika jamii. Anasema si kwa sababu yeye ni mwanamke mwenye uthubutu tu bali kwasababu anajiamini na anaweza kutoa mchango wenye tija katika ulingo wa uongozi. Ni vyema kwa vijana kutoangalia elimu peke yake, ni vyema kupata ujuzi.
‘Niliandika kuomba kazi ya ubalozi Umoja wa Afrika nikiwa najua fika sina kigezo cha shahada ya uzamili, lakini nilisema kwa sababu ukiomba kazi kuna kupata na kukosa, niliandika tu kujaribu na kujiamini kuwa naweza.’
Aidha nafasi hiyo ya ubalozi wa vijana imempa fursa ya kuweza kuongea mbele ya viongozi wakubwa jambo ambalo anajivunia na kuona kuwa vijana wakiaminiwa wanaweza.
‘Ninaamini nikiwa nafanya kazi vizuri, vijana wenzangu pia watapewa fursa hivyo mimi ni ninajiona kuwa ushuhuda na njia kwa wengine.
Kujitolea ni jambo muhimu sana, wakati ninasoma nilikuwa ninajitolea kwenye asasi kama Yuna, tunapanda miti na vitu vingi bila malipo lakini kwenye wasifu wangu ninaandika kila kitu na imenijenga.
Kuna Watoto wengi wanasoma hata nje ya nchi lakini wanasoma tu darasani na kurudi nyumbani yani hawajiongezi. Kiukweli, Kujiongeza kumechangia mafanikio yangu
No comments